RSS
Aside

Mafuriko

Nchi ya demo – ghasia

‘Nchi imetiwa Giza  nasema mimi Mswahili’

Ninaandika kitu kama kitabu lakini wacha niwamegee waswahili wenzangu machache yaliyomo, maana siku za mtanzania zinahesabika na si ajabu ukasikia mswahili hayupo na pengine usisikie lakini ukajua kuwa hayupo maana hutamuona. Katika huo mfano wa kitabu kuna sehemu nimeiita Mafuriko nilikuwa naizungumzia hali ya nchi na urithi wa imani kwa watoto wetu wa leo na wa kesho.

‘Tumepigwa ugenini na nyumbani’ hivyo ndivyo nilivyomsikia jirani yangu Abdallah Punje analalamika akimaanisha tumefungwa mechi zote ya ugenini na ya nyumbani. Nililikamata gita langu nikazivuta siku zijazo nikazilinganisha na hizi zilizopo nikatengeneza maisha ya siku hizo leo. Nikaimba, niliimba weeeh sauti ikakauka, nitaimba tena sauti ikirudi. ‘Tumepigwa ugenini na nyumbani’

Mvua

Mi naapa hii wala sio yetu, hii mvua sio yetu, imetunyeshea  basi tu!

‘Wingu limetanda Magharibi tunanyeshewa sisi Mashariki’ nilicheka sana kwa maana ya kwangu na sio ya msemaji nikizani kuwa msemaji anamaanisha kuwa ‘Wingu limetanda Jioni tunanyeshewa sisi Asubuhi’ kumbe nimenoa, pamoja na kutambua kuwa magharibi ndipo linapotua na Mashariki ndiko lichomozako Jua, na kujiridhisha kuwa anamaanisha wingu limetanda Jioni ‘magharibi’ tumenyeshewa sisi Asubuhi ‘mashariki’ maana ya maneno nimeitambua utata ulikuwa kwenye kujua maana ya maana, maana ya maana bado inasumbua. Labda anamaanisha kuwa Wingu limetanda nchi za Magharibi lakini mvua inatunyeshea sisi huku kwetu, nahisi itakuwa hivyo ndio maana akasema mvua hii si yetu. Tutaharibu mbegu bure tukijifanya wapandaji kwa mvua isiyo yetu.

KUDU

‘Kudu ukudulie umande Masika haikuduliwi’ waswahili wanasema na walisema zamani. Katika utoto wetu tuliwahi kuimba ‘mvua njoo katalina usije’ nikafikiri kuwa maana yake ni mvua njoo Radi usije, na radi tuliyokuwa tunaiogopa sisi ni Ngurumo, mwanga ulikuwa si kitisho kwetu. Miaka michache ya nyuma huko nchi za Asia kumetokea Kimbunga wanakiita Katrina kimezua mafuriko na uharibifu mkubwa wa watu na mali zao, nikashtuka na kujiuliza huyu Katrina ndiye yule Katarina tuliyekuwa tunamuimba asije ije mvua tu? Na kama ndiye huyu mbona wataalamu wanasema kimbunga kama hiki hakijawahi kutokea Duniani miaka mia nyingi zilizopita, inakuwaje leo miaka ya alfu tisa mia themanini mtoto wa kiafrika anaiimba? Hili niwaachie wataalamu wa historia walichimbe mimi wacha niendelee na haya yangu

Kudu ukudulie umande Masika haikuduliwi’  

Huu ni msemo wa Thadhari, mliozoea kuona vimaji kwenye nyasi mkavikudulia hii ni zaidi ya masika.

Umande wa kwenye nyasi waweza ‘ukaukudulia’ ukunyanyua nguo yako ukapita lakini kuna Masika, si mvua ya kitoto, huacha nyasi zimelala au kuchanika chanika. Hupiga mchana kutwa na usiku kucha. Huombwa kwa Sadaka, kafara  na matambiko ikichelewa kufika na masika inapoanza wakulima huwaambia watoto wao wacheze kwenye mvua kufurahia ujio wake, kuonesha kuwa wameikubali na kuiomba isiwakimbie, na watu wanaoikimbia mvua hufukuzwa kijijini maana wanaonesha kuikataa. Natia msemo wangu kidogo  ‘Mkulima hakimbii mvua’

Lakini tusisahau Wakulima wa Mpunga na wa Chumvi hawaivi

Mmoja aomba mvua mwingine aomba jua, usione vitu vinapatana kwenye sufuria ukafikiri huko vitokako kuna amani. Utachekwa.

Sisi watumiaji wa chumvi na mpunga tuna sababu ya kufarakana kwa mambo tunayozani tunayajua na hatuyajui? Tutaishia wapi? Kula wali bila chumvi au kubwia chumvi tupu? Labda nimezungumza lugha ngumu ngoja nizungumze tafsiri ya haya baadhi ya haya, labda nasema kitu kingine ambacho unaweza kuking’amua lakini pia nina maana ya kuwa Migogoro ya tofauti za kiimani si yetu bali inapikwa huko mbali na inatuathiri sisi huku, akili ni nywele sikukatazi wala sikushawishi kujihusisha, amua mwenyewe kwa uwezo wako wa kufikiri na mwisho utakuja kujua kama kujihusisha au kutojihusisha kwako kulikuwa kwa namna gani na kumeisaidia nini asili yako na Nchi yako na ndugu zako. Nanyi viongozi mnatuambia nini juu ya hili? Nyinyi mnajua la kufanya maana kabla hamjajihusisha nyinyi mnahusika sasa kabla hamja litatua msitumie vibaya ndimi zenu maana kauli ya mzee ni dawa.

Kudu ukudulie umande Masika haikuduliwi’  ‘Wingu limetanda Magharibi tunanyeshewa sisi Mashariki’ Hii mvua si yetu mashamba yaandaeni lakini msirogwe kupanda mbegu. Nawaambia mimi Mswahili.

 
1 Comment

Posted by on February 21, 2013 in Uncategorized

 

Waraka

WARAKA wa I 2011

Kwa WAAFRIKA wote ukianzia na Tanzania, Nchi nzuri, chachu ya ukombozi wa Bara la Afrika, kimbilio la wakimbizi wa vita, tamanio la wabakaji wa uchumi.

Nakala hii kwanza iwafikie kwanza watanzania wote kupitia vyombo vya habari, kwaajili ya Bara la Mungu, enyi baadhi ya wanahabari wanafiki, wekeni unafiki wenu pembeni mmjiunge na wenzenu wasio wanafiki kuijuza Dunia Mswahili anaiambia nini Afrika na watu wote.

“Naapa kwamba sitamdhuru kiumbe wako huyu MSWAHILI kwa ujumbe ninao usoma leo hapa, na hata kama maneno yake yatakuwa shubiri kwangu, nitayatumia kwa manufaa ya nchi yangu na watu wangu nikijaribu kufanya kinyume na kiapo changu dhamira yangu mbaya inidhuru. Mungu nisaidie!”

Ndugu,

Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Waziri mkuu, Mheshimiwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mawaziri wote wa kawaida, Mawaziri Vivuli na viongozi wote wa kiimani na kisiasa. 

Heshima yenu popote mlipo!

Mswahili nawasalimia!

Mimi ni Vitali Maembe, mwanamuziki, Mswahili, Mwalimu na mtumishi mwenzenu wa waafrika.

Mnamo tarehe 03/02/2011 nilianza ya kugawa chanjo ya Rushwa, ubinafsi na uvivu kwa kutumia muziki kwa watu wote. Bila kutumwa wala kushinikizwa na mtu wala shirika, wala chama, nilianzia Bagamoyo, mitaani, viwanjani na katika shule njiani kuelekea Dodoma. Ilinichukua siku na wiki kadhaa kufika huko, namna ya kusafiri kutoka kituo mpaka kituo, ruhusa ya kufanya maonesho, vitisho, njaa vilikuwa vikwazo vikubwa.

Hatimaye jumatano tarehe 16 februari 2011 saa nne kasoro dakika kumi natatu mimi na rafiki zangu  wawili tulifika Dodoma kituo kikuu cha mabasi. Lengo likiwa ni lilelile kuiokoa nchi yetu kwa jasho letu, akili yetu yote, moyo wetu wote na uwezo wetu wote kwa kadri tulivyoaminiwa na waswahili wenzetu, kwa kufikisha Waraka wa Chanjo wenye kurasa tano wenye ushauri na unaowaomba mawaziri na wawakilishi wafikirie namna ya kufanya marekebisho kadhaa yatakayoboresha huduma muhimu katika jamii. Ukosefu na uhaba wa huduma na haki unapelekea watanzania wengi kushiriki na kushirikishwa katika Rushwa. Hali ambayo inafanya waswahili tunatukanwa, tunatukana, kutukanishwa na kujitukanishwa, thamani ya utu wetu kutoonekana  ndani ya nafsi zetu na nje katika kuishi kwetu, kwa kifupi sisi waathirika wa rushwa tunajiona kama mifugo tu kwenu nyinyi na wakati wowote mkiamua lolote mnatufanyia, tena mmeshafanya mengi kwa manufaa yenu na mifumo yenu bila kujali uwepo wetu” 

Pia lengo lilikuwa ni kuwasilisha ujumbe kwa njia ya muziki, ujumbe ambao niliagizwa na watanzania wa kawaida.

Pamoja na kufika Dodoma hiyo jumatano ya tarehe 16 februari, hatukwenda moja kwa moja bungeni, tulipumzisha akili zetu, tukasema na njaa zetu, baada ya muafaka tarehe 17 asubuhi tulienda bungeni kuomba ruhusa kumuona Spika wa bunge ili kukabidhi waraka na kopi za albamu ya muziki ya Chanjo. Siku hiyo hatukufanikiwa kupata ruhusa, baada ya usumbufu mkubwa na vitisho getini kutoka kwa askari na wahusika wengine wa mlangoni jioni iliingia na siku ikaisha bila ruhusa. ‘haya ninayoyoyasema naamini mnayajua au mna taarifa nayo’ Hatukukubali kuondoka mpaka tulipopata ruhusa ya kukutana na msaidizi wa Spika Bw. Berege, hatukuweza kumkabidhi barua zetu sitini na nne zinazotakiwa kuwafikia mawaziri wote, wawakilishi wa vyama bungeni, spika na katibu wa bunge kwa kuwa msimamo wetu ulikuwa ni kumfikishia Spika na kumkabidhi ili kuhakikisha ujumbe unawafikia wahusika. Siku iliyofuata yaani tarehe 18 februari 2011, tulifika mapema asubuhi, mara hii tulipata ruhusa ya kuingia katika ofisi ya spika, haikuwa rahisi kuonana naye lakini tuliridhika na ukweli, hivyo tulikutana na Katibu wa spika Bw. Eliufoo na kumkabidhi ujumbe wetu aliupkea saa nne na dakika kumi na sita na akaandika na kuweka sahihi kwenye katatasi yetu nyeupe ya A4 aliyoamua kuikunja katikati kwa mapana baada ya kuandika kwa kalamu yake ya wino wa buluu kuwa amepokea ujumbe wetu.

Awamu ya kwanza ya Chanjo iliishia BASATA Baraza la Sanaa la Taifa. Watu wasiopungua Elfu Ishirini wamekwishapata Chanjo ya Rushwa, Ubinafsi na Uvivu.

Pamoja na hayo yote mpaka sasa sijapata matokeo ya ujumbe wangu Dodoma kutoka kwenu walengwa wote yaani wawakilishi wa vyama na Mawaziri wote. Spika na katibu wa bunge pia mmekaa kimya.

Sasa nawauliza hiyo ni dharau, kiburi au chuki? Na kama ni hasira au chuki mmeniwekea mimi au wananchi wenu?

Sikilizeni niwaambie,

Mnaweza kujiuliza kwanini nitumie gharama nyingi ya muda, pumzi na pesa yangu masikini kama mie na kung’ang’ania kuimba nyimbo za namna hii na kuwafikishia watu moja kwa moja, kueleka bungeni. Kwanini natumia pesa ambayo ingebidi niitumie kuwatunza wanangu wadogo nyumbani wanaosubiri msaada wangu, mimi ni mjinga? Mimi siijui raha ama sina haja ya kustarehe?  kwanini nisifanye biashara ya muziki nikawa tajiri kama hao wanamuziki wengine mnao wafagilia? Kwanini nisiwapigie kampeni niwe mmoja kati yao wanaoahidiwa viwanja ili wawadanganye masikini waswahili hali wakijua ukweli ni upi? Sina kingine  zaidi ya mapenzi kwa nchi yangu na Afrika yangu, tumia akili na umri wako sasa kuelewa mambo mengine.

Lazima ufahamu kuwa Rushwa ndio asili ya mateso wanayoyapata watu wenu, amua leo, sema neno moja tu na watu watapona. Kwa taarifa yako mkuu, watu wanakuficha mimi nakuambia ukweli, Waswahili wanasema huwezi kuwafanya lolote wala rushwa na wezi wa nchi hii kwa kuwa wewe ni mwenzao mimi siamini hayo lakini waswahili wana misemo yao kama vile ‘Lisemwalo lipo…’ au ‘ngoma ikivuma sana…’ nk.. Wewe waswahili unawajua naomba uyatilie thamani maneno yao.

Wakuu!

Nilipoona kuwa kazi yenu ya kuongoza ni ngumu nikaona niwasaidie kurahisisha mambo fulani, lakini mnaniona mpumbavu kabisa, angalieni matusi mnayotukanwa, watu wanailaani siku waliyoenda kupiga kura kuwachagua. Mimi na waswahili wenzangu tumegundua kuwa nyinyi ugumu wa maisha haya ndio raha yenu, mateso ya watu hawa wanyonge ndio matumaini yenu ya maisha bora kwenu, na watoto wenu siku za mbeleni..

Nasema haya maneno yanayoshabihiana na lawama kwenu kwa kuwa naiona juhudi yenu ya kuwafanya watanzania wasisikie muziki wetu, muziki wa mswahili, muziki unaoeleza maisha halisi kabisa ya muafrika na kutoa ufumbuzi.

Tazama! Unawaunga mkono watu ambao wanaonekana wazi hata kwa macho ya kitoto kuwa hawana mapenzi ya kweli nasi, unatuuza watu wako kwa ushawishi wa vitu vidoogo kabisa katika maisha, Makaratasi, makaratasi tu ndiyo yanayokufanya utuone bidhaa, unampa shetani damu ya wanao! Unaiunga mkono kauli ya yule punguani mmoja wa Afrika ya kusini miaka 1980! Umesahau kabisa KIAPO chako kwa Mungu mbele ya Muumba na waswahili wote, umewasahau wazee wetu walivyoteseka na kudhalilika katika kuijenga Afrika hii?

Nakukumbusha!

Yule punguani wa Afrika ya kusini alivyosema,

“The black is the raw material for white man. So Brothers and Sisters, let us join hands together to fight against this Black devil. By now every one of us has seen it practically that the Blacks cannot rule themselves. Give them guns and they will kill each other. They are good in nothing else but making noise, dancing, marrying many wives and indulding sex. Let us all accept that the Black man is the symbol of poverty, mental inferiority, laziness and emotional incompetence”

Je, kwa haya mnayotufanyia leo hali mkiwa wasomi na mnajua yote haya mnafikiri uongozi wenu haukubaliani na huyu bwana? Je, mnawezaje kumshawishi mswahili akawaelewa kuwa hamtumii msimamo huu kuwaongoza waswahili?

Mswahili haitaji majibu ya ahadi bali vitendo na kauli thabiti itakayompa uhuru wa kweli katika ardhi ya babaake.

Tumewapa nguvu ya kutosha itumieni kutuokoa! 

Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Waziri mkuu, Spika wa bunge la Jamhuri ya muungano Tanzania, Mawaziri wote halisi na vivuli.

Najisikia vibaya kukupa ushauri huu lakini inabidi nikupe ingawa ni aibu kwangu na watanzania wote tuliokuweka madarakani, haya mambo ilibidi uwe umeyapitia na kuyafahamu miaka mingi iliyoita na kuyatumia kama ufahamu kukurahisishia nakuiboresha kazi yako ya kuwaongoza watu ambao wameletwa kuishi Afrika ili wasipate taabu, wafurahie maisha katika nchi waliyopewa na Mungu wao.

Sikiliza Mzee wangu!

Uliamua kuiongoza afrika na ukapewa ridhaa na waafrika, usikurupuke tu ukaanza kuongoza bila kujua wapi afrika inatokea, achana na hayo mavideo za ulaya na misimamo ya kigeni, acha kujiamini na elimujoho TANZANIA NI MOJA NA HAKUTAKUJA KUWA NA TANZANIA NYINGI ZAIDI YA HII YA WASWAHILI. Tanzania ndio Afrika, Afrika ndio dunia. Kama utafanya watanzania wakuone bora basi wewe utakuwa bora kuliko viongozi wote Duniani kwakuwa watanzania ni waswahili na waswahili wanafikiria mara tatu ya mtu wa kawaida.Tuliza akili mkubwa unisikilize.

kwa kukusaidia tu ni kwamba ujue kuwa  huna uwezo wa kuiongoza hata sehemu ndogo ya waafrika pekeyako, tena bila kujua haya nikwambiayo leo ndiyo kabisaa.

Niwie radhi mkubwa wangu kama utaona nakukosea kukwambia haya. Sikwambii haya kukushusha cheo chako, la, haya ni mapenzi tu. Nakuomba uupe heshima umri wangu, na kazi yangu kama mwanamuziki, mwalimu na mswahili kwa kusikia mafundisho yangu.

Kuna kitu kinaitwa Pan-africanism.

Ndani ya hiyo tafuta kujua kuhusu wanasiasa wake, viongozi, wanamuziki na watu wengine waliohusika na afrika kwa moyo wao wote. Mwanao nakuomba uyashike haya, kama huwezi kuhifadhi kichwani shika kalamu na uandike haya. Wengi wa hawa walifanya mambo mazuri lakini mimi nawewe hatujui nia za moyoni mwao, pia wapo wliofanya mabaya, kwa kuangalia walikoanzia mpaka wanakoishia utajua lipi linalokufaa.

Nenda ukamsome.

Nnamdi Azikiwe, Robert Mugabe, Amílcar Cabral, Muammar al-Gaddafi · Marcus Garvey, David Comissiong, Kenneth Kaunda, Samora Machel, Jomo Kenyatta, Patrice Lumumba, Thabo Mbeki, Abdias do Nascimento, Gamal Abdel Nasser,  Oliver Tambo, Kwame Nkrumah, Julius Nyerere, John Nyathi Pokela, Haile Selassie, Robert Mangaliso Sobukwe, Ahmed Sékou Touré, Abdulrahman Mohamed Babu, I.T.A. Wallace-Johnson

Usiache kumsoma.

Molefi Kete AsanteSteve BikoEdward Wilmot Blyden, John Henrik Clarke, Cheikh Anta Diop, W. E. B. Du Bois, Frantz Fanon, John G. Jackson, Yosef Ben-Jochannan, Maulana Karenga, Fela Kuti, Bob Marley, Malcolm X, Ibrahim Hussein, Zephania Mothopeng, George Padmore, Motsoko Pheko, Runoko Rashidi, Walter Rodney, Burning Spear, David G. Mailu, Henry Sylvester-Williams, Stokely Carmichael, Omali Yeshitela

Tuliza akili yako ujue wamefanya nini na wamefanyiwa nini kwaajili ya afrika yao na kwaajili yao binafsi.

Usije ukawaongoza waafrika bila ufahamu mkubwa kuhusu haya yafuatayo, hapa ndipo kuna malengo, nia, utu na heshima yetu. Kuchanganyana na kuchanganyikana.

United States of AfricaAfrocentrismKwanzaaPan-African coloursPan-African flag,  Négritude ,African nationalismAfrican socialismAfrican Century · AfricanizationKawaidaUjamaaHarambee, UbuntuZikismBlack nationalism.

Jua na uelewe kuhusu muungano, mabadiliko, umoja wetu na kudumu kwetu kama waafrika.

African UnionOrganization of African UnityUhuru MovementUNIA-ACL · African Unification FrontInternational African Service Bureau.

Hayo mambo mengine ni urembo tu, ni njia ya kutafuna rasilimali za waafrika tu. Nakuamini sana na ninaamini kuwa maneno yangu yatawasaidia watanzania na waafrika wenzangu kupitia busara zako, hayatakuwa chanzo cha wewe kunitesa au kugeuka sababu kuniua masikini mie ninayejaribu kuwakoa watanzania na waafrika wenzangu. Najua nimekupa nguvu ya kufanya lolote utakalo lakini naomba usinidhuru kwani wanangu na wapenzi wangu bado wananihidaji.

Mimi ni wanamuziki nisingependa haya yafikie huku lakini imebidi nitumie njia hii maana nimeimba sana lakini redioni hawapigi, wengi wao wanasema wanahofia utawala wenu, hautafurahia nyimbo za mafunzo, lakini labda ni uoga wao tu, nakuomba uwaruhusu basi wapige nyimbo za Vitali Maembe.

Mkuu,

Katika kuongoza yashike hayo yote lakini langu mimi ni moja tu kama si mawili, usiupe nafasi ubinafsi, ubaguzi wa rangi, dini, kabila na jinsia.

Mwisho,

Usiache muziki ukadhalilishwa, usiupromoti muziki ambao unaona wazi unawapeleka watu wako pabaya, nchi italaaniwa, Muziki mzuri ni ule unaotoa elimu njema na kuwasaidia watu, ule mwingine usiuue pia uache uwepo tu ili kutofautisha kizuri na kuzuri sana. ‘pasipo ndicho kilichopo ndicho?’

Mswahili anakutakia uongozi mwema na mafanikio katika mema!

‘Mungu ulisha ibariki Tanzania, Mungu ulisha ibariki Afrika! Tunaomba usituondolee Baraka hii!’

“Hakuna kuogopa, hakuna kuongopa!”

Vitali Maembe. 2011

 
2 Comments

Posted by on March 28, 2011 in Waraka

 

Chanjo

Mwanzo wa Chanjo

Mwanzo wa Chanjo

Mara nyingi imezungumzwa na kujengeka katika jamii yetu ya watanzania, pia hata jaamaa zetu nchi za jirani kuwa Rushwa ni jambo ambalo halitaisha, wengine wanathubutu kusema kuwa dunia hii bila rushwa si dunia.

Rushwa imewafaa wabinafsi wengi, imewanufaisha na kuwadhalilisha watu wengi katika jamii mbalimbali Duniani, imefanywa kuwa ni kitu cha muhimu kabisa katika maisha yetu.

Tunaisema vibaya na kuiandika vibaya rushwa kutokana na ubaya wake, wakati mwingine tunafanya hivyo ilitupate kibali kwa watu au kuungwa mkono na wanyonge au waathirika wa rushwa, lakini kusema ukweli ndani yetu bado hatujakubali ukweli ambao wote tunaujua kuwa rushwa ni tatizo.

Tangu kiongozi mkubwa wa kisiasa mpaka mtu wa kawaida kabisa katika jamii anaamini kuwa rushwa haitaisha, watu wanaishiriki rushwa kwa sababu fulani, wakati mwingine kwa kuamua na wakati mwingine kwa kulazimika. Ninaamini kuwa rushwa ina mwisho, nitaendelea kuamini hivyo kwa kuwa huo ndio ukweli wenyewe.

Ingawa nyimbo za kuwaweka huru watanzania kutoka katika makucha ya rushwa zinaonekana ni hotuba ya mwendawazimu tu.

Rushwa imesimama imara kwa kujiamini, mawakala wake wamekuwa na nguvu kupindukia. Wasanii na wana habari ndio tumaini pekee la ukombozi wa mtu wa kawaida dhidi ya rushwa, lakini baadhi yao ndio wamekuwa mawakala wa rushwa, hatupendi kusema maneno haya lakini inapobidi inabidi tuseme ingawa tunajuwa tutaumizwa kwa kusema haya. Wazazi wamekata tamaa, walezi wa kiimani na kimaadili wanasema “rushwa haiepukiki na hivyo ndivyo ilivyo tutafanyaje?”

Naishi katika mazingira ambayo watu wanalia kila siku, wanalalamika kilasiku kuhusu rushwa, watu ambao wanashindwa kumudu matibabu, watu ambaowanashindwa kupata huduma ya elimu ipasavyo, watu wanaopoteza maisha yao na jamaa zao kutokana na upevu wa rushwa. Siitazami tena rushwa kwa macho ya kawaida, naitazama kwa roho na naichunguza tabia yake ninagundua kitu.

Nikawatazama watanzania, nikawatazama waafrika, nikaitazama dunia sioni tena umuhimu wa nyimbo za kuwaburudisha na kuwapumbaza watanzania, kwa hali iliyopo siwezi kusema wasanii wote tubadilike bali wanaoweza kusema na njaa zao wafanye hivyo na tuangalie ni namna gani tunaikoa nchi yetu na sio ni namna gani tunajinufaisha kifedha.

Siogopi tena kusema kwamba naifahamu rushwa vilivyo, nayajua madhara yaliyoletwa na rushwa, nayajua maafa yatakayoletwa na rushwa, nawajua mawakala wa rushwa, zaidi na zaidi naujua umri wa rushwa, nathubutu kukwambia ukweli huu, kitu bora na cha ajabu ni kwamba kifo na uhai wa rushwa vipo katika ulimi wangu, vipo katika akili na roho yako.

Bado kidoogo sana tutamjua nani ni mwanamapinduzi wa kweli.

Huu si wakati wa nadharia, kama tunaitakia mema jamii yetu, Siafu waliamua kujenga daraja kwa miili yao, kwa kushikana na kufungana wenzao waliweza kwenda upande wa pili kwa kupita juu yao…. Wanajulikana kwa matendo yao kamwe si maneno yao.

Leo hii nakupa CHANJO dhidi ya rushwa na ubinafsi, nakupa uwezo wa kusema ‘rushwa kufa’ na rushwa ikafa.

Nimepita redioni na kugawa miziki ili uisikilize kwa makini, ipenye roho na akili yako kupitia masikio yako na iwe kinga yako dhidi ya rushwa. Wengi walifikiri kwamba hizi ni hadidhi tu, la haya ni maisha halisi.

Nimepita katika shule na mitaa ya Bagamoyo, nimekaa na watu na kuwapa chanjo kwa kuwapigia muziki, kukaa na kujadili nao juu ya janga hili.

Mnamo tarehe 03/02/2011 nilianza kazi hii bila kutumwa wala kushinikizwa na mtu wala shirika lolote. Majira ya saa tatu kamili kazi hii ilianzia katika shule ya msingi Mbaruku, kisha Mwanamakuka, kisha Majengo, kisha shule ya sekondari Dunda, na baadaye kumalizia na shule ya msingi Jitegemee. Watoto, wanafunzi wasio pungua 2000, walimu wasio pungua 9 walipata chanjo na kula kiapo cha kuikataa rushwa. Tarehe 04/02/2011 niliendelea katika shule ya msingi Pande, kisha shule ya msingi Mwambao, wanafuzi wasiopungua 500, walimu 7 walipata chanjo na kula kiapo.

Tarehe 05/02/2011 nilifanya onesho katika eneo la wazi Bagamoyo mjini kwenye viwanja vya Toptop, wakaazi wa bagamoyo wa umri tofauti tofauti wasio pungua 1000 walipata chanjo.

Tarehe 08/02/2011 nilikwenda shule ya sekondari ya Kiromo, wanafunzi 600 walimu na wafanyakazi wa shule 6 walipata chanjo na kula kiapo cha kuikataa rushwa. Jioni ya tarehe hiyo nilimaliza kwa kuwapa chanjo wanachuo TaSUBa na wakazi wa jirani na chuo hiki cha sanaa bagamoyo wasio pungua 400.

Safari hii iliaendelea mkoa wa Dar es salaamu, kisha tena Pwani, Morogoro, mpaka Dodoma. Panapo majaaliwa tutafika Singida, Tanga na Kilimanjaro.

Tarehe tulifika Dodoma kwa lengo la kufikisha Waraka wa Chanjo wenye kurasa tano unaowataka mawaziri na wawakilishi wafikirie namna ya kuboresha huduma katika jamii ambazo zinapelekea watanzania wengi kushiriki au kushirikishwa katika Rushwa. Pia likuwa ni kuwasilisha ujumbe kwa njia ya muziki, ujumbe ambao niliagizwa na watanzania wa kawaida. Mimi na wenzangu watatu tulifika Dodoma jumatano ya tarehe 16 februari, tarehe 17 asubuhi tulienda bungeni kuomba ruhusa kumuona Spika wa bunge ili kukabidhi waraka na kopi za albamu ya muziki ya Chanjo. Siku hiyo hatukufanikiwa kupata ruhusa, baada ya usumbufu mkubwa na vitisho getini kutoka kwa askari na wahusika wengine wa mlangoni jioni iliingia na siku ikaisha bila ruhusa. Hatukubali kuondoka mpaka tulipopata ruhusa ya kukutana na msaidizi wa Spika Bw. Berege, hatukuweza kumkabidhi barua zetu sitini na nne zinazotakiwa kuwafikia mawaziri wote, spika na katibu wa bunge kwa kuwa msimamo wetu ulikuwa ni kumfikishia Spika na kumkabidhi ili kuhakikisha ujumbe unawafikia wahusika. Siku iliyofuata yaani tarehe 18 februari 2011, tulifika mapema asubuhi, mara hii tulipata ruhusa ya kuingia ktk ofisi ya spika, haikuwa rahisi kuonana naye lakini tuliridhika na ukweli, hivyo tulikutana na Katibu wa spika Bw. Eliufoo na kumkabidhi kwa maadishi.

Pamoja na hayo yote mpaka sasa sijapata matokeo ya ujumbe huo kwa walengwa wote yaani wawakilishi wa vyama na Mawaziri wote. Spika na katibu wa bunge pia wamekaa kimya.

Yawezekana wanafikiri kuwa huyu ni mpuuzi fulani anajaribu kujifurahisha au hawajaona umuhimu wa huu ujumbe kwao maana wengi wao kitu kizuri na chema kinasemwa na mtu fulani na sio Vitali Maembe, mtoto yatima fulani ambaye Baba yake alikuwa mtumishi mdogo tu wa Serikali ambaye baada ya kufa kwake hata mafao yake yameonekana kuwa hayastahili kwenda kwa mwanae sababu ya unyonge wa kielimu wa yatima huyu na ubabe wa kirushwa wa mifumo yao . Lakini wangejaribu kufikiri ni nani aliwahi kuandaa albamu ya muziki ili kuinusuru Tanzania na Afrika yake bila msaada? Au ni nani aliwahi kusafiri mtaa hadi mtaa. Kijiji hadi kijiji, Mji hadi mji akijaribu kuwaelimisha watanzania wenzake na kuwapa moyo wa matumaini naujasiri bila kuwa na ufadhili wa kifedha?

Au mtu huyu anatoka katika maisha gani? Vitali Maembe anatoka katika azingira na maisha wanayoishi watanzania wengi, anajua nini anachoongea, anaongea kitu kinachosemawa na wtanzania wa sasa.

Wenye akili wanaweza kusema nini matokeo ya hii dharau iliyoonyeshwa na Spika, Mawaziri, wabunge na baadhi ya watu waliopata walaka huo ulioambatana na albam ya Muziki ulio andaliwa ili kuwasaidia kuingoza nchi hii nzuri.

Tukiachana na hao Viongozi wetu,

Ndugu watanzania wenzangu,

Nimemaliza awamu ya kwanza ya kugawa Chanjo kwa kufanya onesho Baraza la sanaa tarehe 28 februari 2011. na kufikisha idadi ya watu wasiopungua 20,000 wakiwemo Wanafunzi, walimu, wanasiasa, wazazi, wanahabari, wasanii na watu wa kawaida wamepata Chanjo dhidi ya Rushwa, Uvivu na Ubinafsi.

Pengine inaweza kuwa kazi ngumu sana kulimaliza hili tatizo kwa muda mfupi lakini mimi nawe tukikubali kuwa rushwa ni tatizo, tukianza leo kulitatua tunaweza kuijenga Tanzania bora.

Kwa utafiti nilioufanya kwa kina sisiti kusema kuwa huu ndio wakati pekee ambao tuna weza kuikoa nchi yetu kwa Kalamu na Midomo yetu, tukisubiri kitambo hiki kipite watoto wetu watatakiwa kuiokoa nchi hii kwa gharama kubwa sana, sipendi kulitaja neno damu lakini huko ndiko tunakoelekea. Bado hatupaswi kufikia huko maana kama sisi tukikubali kuumia kidogo leo tutaepusha maumivu makubwa kwa watoto na wajukuu zetu.

Mimi leo nakupa nyimbo zisizopungua 14 kwenye albam ya Chanjo, nakupa nyimbo zisizopungua 32 uzisikilize na ziwe chanjo kwako, napita mtaa hadi mtaa, shule hadi shule, bila ghrama yoyote njoo upate chanjo ili tuliokoe taifa letu.

Naamini kuwa kama nitakubali kumwaga Jasho langu leo, kesho mwanangu hatomwaga damu. Siamini katika pesa, siamini katika mali, bali naamini katika ukweli. Nitaimba kwaajili ya nchi yangu mpaka wasioelewa waelewe. Ungana na mi kama una mapenzi mema na nchi hii. Pata chanjo eneza chanjo… sikiliza muziki wa Vitali Maembe, hudhuria maonesho ya Vitali Maembe leo wakati huitaji kutoa lolote ili upate elimu au burudani.

Mungu ulisha ibariki Tanzania, Mungu ulisha ibariki Afrika, chonde usituondolee Baraka hii.

 
7 Comments

Posted by on March 18, 2011 in Chanjo tour

 

Tags: , , , , , , , , , ,